GuidePedia

0


JUMUIA ya wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Nkasi mkoani Rukwa imetoa msaada wa magodoro 50 kwa Wanafunzi wa kike wanaoishi hostel katika shule ya sekondari Mkwamba na kuondokana na adha ya kulala chinimi.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo katibu wa jumuia ya wazazi CCM wilayani Nkasi  Bashiru Kambarage  amedai kuwa jumuia hiyo imelazimika kutoa msaada huo baada ya kujionea changamoto ya watoto hao wa kike walipoitembelea shule hiyo wakati wa sherehe za jumuia hiyo ya wazazi ambazo kimkoa zilifanyika kata hiyo ya Mkwamba ambapo waliweza kujionea mazingira magumu wanayoishi watoto hao kwa kulalia misengele na mifuko ambayo imefunikwa kanga.

Alisema kufuatia hari hiyo CCM iliahidi kuwapatia  wanafunzi hao wanaoishi hostel magodoro 25 na kuwa baada ya kurudi ofisini waliona kuwa idadi hiyo ya magodoro ni ndogo na kuamua kutoa magodoro 50 ambayo sasa ameyakabidhi ikiwa ni pamoja na Tshs,155,000 ambazo zitatumika kununulia pazia za kwenye mabweni ya wanafunzi hao ikiwa ni pamoja na vioo kwa ajiri ya madirisha ambayo yamepasuka.

Katibu huyo wa jumuia ya wazazi alidai kuwa mazingira wanayosomea wanafunzi  katika shule hiyo ni magumu hususani kwa watoto wa kike na kuwa ili kuweza kukabiliana na mimba mashuleni kulingana na mazingira yenyewe ni azima watoto hao wa kike waishi hostel ambako nako watajengewa mazingira rafiki na kupata fursa nzuri ya kujisomea na kuweza kufanya vizuri kwenye mitihani yao.

Akipokea msaada huo kaimu afisa elimu sekondari wa wilaya Nkasi Fortunatus Kaguo aliishukuru jumuia hiyo ya wazazi kwa msaada huo na kuwa ili mtoto aweze kufanya vizuri na kuwa na maendeleo mazuri ya elimu inahitaji aishi katika mazingira mazuri na kuwa CCM wamelitambua hilo na wao kwa upande wao watauenzi msaada huo kwa kuhaskikisha kuwa vifaa hivyo vinadumu kwa muda mrefu.

Alisema kuwa kazi iliyofanywa na CCM ilibidi ifanywe na serikali na kuwa kwa vile serikali ina mambo mengi ya kufanya inahitaji pia misaada kutoka kwa wadau wengine kuchangia shughuli kama hizo za maendeleo na kuwa jumuia hiyo imeonyesha mfano na kutaka watu wengine na taasisi mbalimbali kujitoa ili kusukuma haraka maendeleo ya elimu hapa nchini.

Kwa upande wake mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo Morris Buberwa alionyesha kufurahishwa na  misaada hiyo na kuwa itawapunguzia kero wanafunzi hao ya kulala chini na kuwafanya wawe na afya itakayowafanya wazingatie masomo yao na kuweza kufanya vizuri.

Awali katika taarifa yao ya shule ya sekondari Mkwamba iliyosoma na makamo mkuu wa shule hiyo Lukuta Andrew ilisema  kuwa shule hiyo ina changamoto nyingi na kubwa ni la watoto kukatishwa masomo yao kwa sababu ya kupata ujauzito na kuwa kwa mwaka huu tu wanafunzi wawili wa kidato cha tatu wamepata  mimba na taarifa amepelekewa afisa mtendaji wa kata lakini wamekuwa hawapati mrejesho wa taarifa juu ya mwenendo wa kesi hizo.

                                         Na, Lumemo blog.

Post a Comment

 
Top